0
Mkuu wa Wilaya (DC)  Kinondoni, Ally Hapi amemwagiza Kamanda wa Polisi mkoa wa Kinondoni, Suzan Kaganda kumkamata mbunge wa Kawe, (Chadema) Halima Mdee na kumweka mahabusu kwa saa 48 kutokana na kutoa maneno ya uchuchezi kwa Rais John Magufuli.

Mdee anadaiwa kutoa maneno hayo ya kukashifu na ya uchochezi katika mkutano wake wa Baraza la Wanawake Chadema (Bawacha) uliofanyika jana katika makao makuu ya chama hicho.

Akizungumza na wanahabari ofisini kwake leo (Jumanne Julai 4) Hapi amesema kauli za Mdee kuhusu wanafunzi waliopata mimba kurudi shuleni, imemshtua yeye kama mwenyekiti wa  Kamati ya Ulinzi na Usalama wa wilaya hiyo.

Amesema ameamua kuchukua hatua hiyo hasa baada ya Mdee, alipomshushia kashfa hizo kiongozi wa nchi ambaye ni Amiri Jeshi Mkuu wa nchi.

 
"Mh. Mdee amemtaja kwa jina rais kwamba ana tabia za hovyo, na kwamba tabia zake za hovyo zimempelekea kuona kwamba maneno yake ndiyo sheria ya nchi. Pia amesema kwamba ipo siku rais ataagiza watanzania watembee vifua wazi yaani wanawake kwa wanaume. Nimeshtushwa sana", amesema Mh. Happi na kuongeza;

 "Maneno yake ni ya kichochezi ambayo hayakubaliki, hayafai kutolewa na kiongozi kama yeye hivyo namuagiza kamanda amkamate Mdee amweke ndani kwa saa 48 ili ahojiwe yale yote aliyoyaongea ili afikishwe kwenye vyombo vya usalama,"

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top