0
Balozi mpya wa Tanzania nchini Sweden, Dk Willibrod Slaa ameapishwa leo Februari 16, 2018, Ikulu Dar es Salaam na Rais John Magufuli na kuahidi kuwa utendaji wake utajikita kwenye diplomasia ya uchumi.

Mbali na Dk Slaa ambaye ni katibu mkuu wa zamani wa Chadema, Rais Magufuli pia amemuapisha Balozi wa Tanzania nchini Nigeria, Muhidin Mboweto.

Rais Magufuli alimteua Dk Slaa kuwa balozi Novemba 23, 2017 na tangu wakati huo alikuwa akisubiri kupangiwa kituo chake cha kazi.

Dk Slaa ambaye tangu ajiuzulu wadhifa wake Chadema amekuwa akiishi Canada, alitangaza kuachana na siasa kutokana na kutofautiana na chama chake katika kumpokea Edward Lowassa aliyehamia kutoka CCM na baadaye kupitishwa kuwa mgombea urais kupitia muungano wa Ukawa.

Alisema chama chake hakikutekeleza makubaliano waliyoafikiana ya kuwapokea baadhi ya makada wa CCM akiwamo Lowassa.

Hafla hiyo fupi ya Ikulu ilihudhuliwa na Naibu Waziri Mambo ya Nje, Dk Suzan Kolimba na Mwenyekiti wa Tume ya Maadili, Jaji Harold Nsekela.

“Tangu nikiwa mbunge na wewe ukiwa bungeni, tumepigia kelele sana ubalozi wa kiuchumi na wewe baada ya kuanza mwaka wa pili, umeanzisha mchakato wa spidi kali katika kila eneo ili kufikisha mahali safari ya kuikuza Tanzania kiuchumi,” amesema Dk Slaa,

“Katika ulimwengu wa leo, pamoja na kazi zile nne zilizozoeleka, diplomasia ya sasa ni ya kiuchumi. Ninakushukuru kwa kunipeleka mahali ambapo naweza kutoa mchango wangu.”

Dk Slaa aliahidi kufanya kazi kwa uwezo wake, akili na kwa nafasi yake yote huku akimwomba Mungu amsaidie kufanikisha dhana ya Tanzania ya viwanda.

“Natambua kwamba maendeleo ni safari na safari yoyote unakwenda hatua kwa hatua. Huwezi kusema unakwenda Mbeya, ukaruka dakika ile ile au sekunde ile ile ukafika Mbeya. Unapiga hatua moja, ya pili unapanda kituo cha kwanza cha pili na tatu,” amesema,

“Ahsante Mheshimiwa Rais kwa kuniona, kwa kuniamini na kunipa majukumu haya, naamini sitakuangusha.”

Naye Balozi Mboweto licha ya kumshukuru Rais Magufuli aliahidi kufanya kazi kwa uwezo wake wote kwa bidii kwa weledi na kwa kuzingatia maadili ya utendaji wa serikali.

Akisisitiza diplomasia, Dk Kolimba amewahakikishia  mabalozi hao ushirikiano katika kutimiza adhama hiyo.

“Jukumu kubwa tulilopewa ni kutekeleza diplomasia ya uchumi na kwa nchi ambazo umewapeleka mabalozi hawa najua watatumia uzoefu walio nao na tutawapa ushirikiano wa kutosha,” amesema.

“Tunataka kuwahakikishia mabalozi hawa wawili walioteuliwa leo sisi kama wizara, tutawapa ushirikiano wa kutosha kwa sababu wao watakuwa sehemu ya wizara.”

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top