0


Image result for TANZANITE 
Serikali imesema itaweka mikakati madhubuti ya kutangaza  madini ya Tanzanite nje ya nchi na kwamba  italifanyia kazi kwa nguvu zake zote suala la madini na kuhakiki mwenendo wa uzalishaji katika machimbo ya madini ya Tanzanite yanayopatikana eneo la Mirerani wilayani Simanjiro mkoani Manyara kutokana na suala hilo kuwa na vikwazo vingi vya kiuendeshaji.

 Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa aliyasema hayo juzi  katika mkutano wa hadhara uliofanyika uwanja wa  Getini katika eneo la Mirerani wilayani humo ambapo  alisisitiza kuwa serikali pia itahakikisha madini ya Tanzanite yanayopatikana Tanzania katika eneo la Mirerani  yanatangazwa na kujulikana duniani kote na kuwanufaisha wajasiriamali wadogo  na wazawa.

 Alisema madini ya Tanzanite yanayopatikana pia India yanajulikana zaidi duniani kuliko yanayopatikana Mirerani,  Tanzania  na kwamba itaangalia upya  ya sheria inayoruhusu makampuni ya nje yanayonunua madini hayo katika ulipaji kodi ili halmashauri  husika ziweze kupata mapato ya ndani na serikali kupata
 mapato kutokana na minada ya madini hayo na uwekezaji.
 
 Alisema imegundulika  kuwa sekta  ya madini ina matatizo mengi  na migongano kati ya wachimbaji wadogo na wakubwa na upatikanaji wa leseni za makundi hayo ambapo  sheria ya madini nchini inasisitiza wachimbaji na wawekezaji  kuwa na leseni jambo ambalo alisema litafanyiwa kazi ikiwa  ni pamoja na kujua wawekezaji wameingiaje katika maeneo hayo, leseni zao zimepatikana wapi na mfumo wa ulipaji kodi wao.

 Waziri mkuu alisisitiza kuwa azma ya serikali ni kuona  inawainua wajasiriamali wadogo wa machimbo ya madini ikiwa  ni pamoja na kuwa na zana bora za uchimbaji kwa kutambulika  kisheria na kwamba ili waweze kufanya kazi hizo za  uzalishaji ni lazima waondokane na maambukizi ya ugonjwa wa ukimwi ambapo alisema katika eneo la Mirerani pekee maambukizi hayo yako juu kwa asilimia 18.

 Aidha aliwataka wazazi na walezi wa watoto waliofikia umri wa kupelekwa shule wanakwenda shule kwa kuwa serikali  imefuta michango ya ulinzi, taaluma, bili za umeme, ada na  gharama za mitihani zilizokuwa zikigharamiwa awali na  makundi hayo ili watoto wengi wakapate elimu ambapo  aliwaagiza maafisa elimu wa shule za msingi na sekondari  wilayani humo kusimamia kikamilifu agizo hilo hasa katika  eneo hilo ambalo watoto wamekuwa wakitumikishwa katika kazi za migodi.
 
 Akiwasilisha taarifa ya wilaya ya Simanjiro  mbele ya waziri Mkuu, Mkuu wa wilaya hiyo Mhandisi Zephania Chaula  alisema kuwa wachimbaji wa madini hayo ya Tanzanite baadhi  yao hawatoi  takwimu sahihi za uzalishaji zinazoiwezesha halmashauri kukusanya kodi ya huduma kutokana na utoroshaji wa madini hayo nje ya wilaya na nje ya nchi.
 
 Kwa upande wake mbunge wa jimbo la Simanjiro James Ole Milya alipongeza juhudi za serikali ya uongozi wa awamu ya tano  katika kujiletea maendeleo ambapo pia alimwomba waziri mkuu
 kuimarisha  miundo mbinu ya barabara na huduma za  kijamii za maji safi na salama ambapo tatizo hilo limekuwa  sugu katika wilaya hiyo.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top