0
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuachia Huru Mfanyabiashara Yussuf Manji na wenzake kwenye uhujumu Uchumi baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka DPP kuwasilisha hati ya kutoendelea na Mashtaka mahakamani hapo.
Akiwasilisha hati hiyo Kishenyi Mutalemwa Wakili wa Serikali mbele ya Hakimu Mkazi, Huruma Shahidi ambapo ameeleza Mkuregenzi huyo hana nia ya kuendelea na Mashataka hayo. Manji alifikishwa kwenye mahakama hiyo majira ya saa 7 mchana akitokea mahabusu. Washitakiwa wengine katika kesi hiyo ni Meneja Rasilimali watu wa Kampuni ya Quality Group Ltd, Deogratius Kisinda (28), Mtunza stoo, Abdallah Sangey (46) na Thobias Fwere (43).
Awali Julai 5, mwaka huu, mahakama ililazimika kumfuata Manji kwenye wodi namba moja ya Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, Muhimbili alipokuwa amelazwa kutokana na ugonjwa wa moyo na kusomewa mashtaka ya uhujumu uchumi.
Aidha alidaiwa Juni 30, mwaka huu maeneo ya Chang’ombe A wilayani Temeke Dar es Salaam, washitakiwa wote kwa pamoja walikutwa na askari polisi wakiwa na mabalo 35 ya vitambaa vinavyotumika kutengenezea sare za Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) vyenye thamani ya Sh. 192.5 milioni .
Pia washitakiwa wote walikutwa na askari polisi wakiwa na mabalo nane ya vitambaa vinavyotumika kutengenezea sare za JWTZ vyenye thamani ya Sh. 44 milioni .
Katika mashitaka ya tatu, inadaiwa Juni 30, mwaka huu maeneo ya Chang’ombe A, washitakiwa walikutwa wakiwa na mhuri wa JWTZ ambao uliandikwa “Mkuu wa Kikosi 121 Kikosi cha JWTZ” bila kuwa na uhalali kitendo kinachohatarisha usalama wa nchi.
Pia inadaiwa tarehe hiyohiyo maeneo ya Chang’ombe, washitakiwa walikutwa na mhuri uliokuwa umeandikwa “Kamanda Kikosi 834 KJ Makutupora Dodoma” bila kuwa na uhalali kitendo kinachohatarisha usalama.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top