0
Displaying 686.JPGWaziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Isdor Mpango, amewataka  Watumishi wa Wizara hiyo kuongeza ukusanyaji wa mapato na kusimamia nidhamu ya matumizi ya Fedha za Umma ili  kuijengea Serikali uwezo wa kuwahudumia wananchi na kuifanya nchi iwe na uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025.
Dkt. Mpango ameyasema hayo Jijini Dodoma wakati akifungua Mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa Wizara hiyo uliowakutanisha wajumbe zaidi ya 190 kutoka maeneo mbalimbali nchini.
Amesema kuwa  Wizara  ya Fedha na Mipango inajukumu la kuhakikisha inatekeleza usemi wa “Wizara ya  Fedha na Mipango ndiyo Moyo wa Serikali” kwa kutumia  Baraza la Wafanyakazi katika kushauriana na kuchangia  mawazo yatakayosaidia katika kutekeleza majukumu ya Wizara kama yalivyopangwa na kusukuma kasi ya maendeleo ya uchumi wa Taifa.
“Watumishi wote wa Wizara mnaowajibu wa kutoa huduma bora kwa wananchi kwa kutumia utaalamu mlionao na kutekeleza majukumu kwa kuzingatia nidhamu, maadili, sheria, kanuni na  taratibu za utumishi wa Umma ili kuongeza tija” alieleza Dkt. Mpango.
Akizungumzia suala la maadili Dkt. Mpango amesema kila mtumishi wa Wizara hiyo anapaswa kutunza siri na nyaraka za Serikali kwa kuzingatia kuwa taarifa zinazopatikana kutokana na majukumu haziachwi ovyo na hatimaye kuangukia mikononi mwa watu wasiohusika.
“Watumishi wote mnapaswa kutotumia nyaraka au taarifa za ofisi za umma kwa masuala ya kisiasa kwani huo ni uvunjaji wa taratibu za utumishi wa Umma”, alisisitiza Waziri Mpango.
Amesema kila mtumishi anao wajibu wa kufanya kazi kwa bidii na kushirikiana kila mmoja katika nafasi yake ili hatimaye Wizara ya Fedha iweze kufikia malengo iliyojiwekea kwa mwaka ujao wa fedha 2018/2019 na kuchangia ipasavyo katika utekezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025.
Dkt. Mpango, amewaagiza watendaji wa Wizara hiyo kuhakikisha kuwa vikao vya Baraza la Wafanyakazi vinafanyika   kama vilivyopangwa kwa kuwa ni sehemu nzuri ya wafanyakazi kueleza changamoto zao na kutoa mawazo namna ya kuboresha utendaji kazi wa Wizara.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Bw. Doto James, amemhakikishia Waziri Mpango kuwa watatekeleza maelekezo yote aliyoyatoa kwa ukamilifu ili kuongeza tija.
Akitoa maoni yake,  Mhakiki mali za Serikali kutoka Mkoa wa Dar es Salaam Bw. Ismail Ugaga ambaye ni mmoja wa wajumbe wa Baraza hilo amesema kuwa umefika wakati ambao Serikali inapaswa kuchukua hatua kali kwa wale wote wanaotoa siri za Serikali ili kukomesha tatizo hilo miongoni mwa watumishi wa umma.
Lengo  kuu la Baraza la Wafanyakazi sehemu za kazi ni kuongeza tija, ufanisi na ushirikishwaji wa wafanyakazi katika uongozi wa pamoja mahali pa kazi kama linavyoagiza Agizo la Rais Na. 1 la mwaka 1970 likisomwa pamoja na miongozo mingine inayoyekeleza agizo hilo.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top