Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
imeshauriwa kuangalia uwezekano wa kutumia Teknolojia Mpya ya
utengenezaji wa Bara bara kwa kutumia maadini maalum ambayo
uchanganyaji wake baadae unageuka kuwa zege linaloweza kudumu kwa
miaka mingi.
Ushauri huo umetolewa na Mratibu Mkuu wa
Kampuni ya Kimataifa ya utengenezaji wa Madini ya Margania kutoka Nchini
Uturuki Bwana Ahmet Nesih ONAL wakati wa mazungumzo yake na Makamu wa
Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Vuga Mjini Zanzibar.
Bwana Ahmet Nesih alisema Bara bara mbali
mbali zinazotengenezwa kwa kutumia Maadini ya Margania zinaipunguzia
Serikali gharama Kubwa ya Fedha sambamba na matumizi mengi ya Vifaa
wakati wa ujenzi wa miundombinu hiyo kwa ajili ya mawasiliano ya usafiri
Mijini na Vijijini.
Mratibu Mkuu huyo wa Kampuni ya Kimataifa
ya utengenezaji wa Madini ya Margania alimueleza Makamu wa Pili wa Rais
wa Zanzibar kwamba Uongozi wa Kampuni yake umeshuhudia ujenzi wa Bara
bara nyingi katika maeneo mbali mbali Duniani zinazotumia mfumo wa Lami
ambao unaweza kuepukwa kwa kupungua matumizi.
Alisema yapo baadhi ya Mataifa Ulimwenguni
kama Qatar, Kuweit, Saudi Arabia na Iraq zilizoanza kutumia Teknolojia
hiyo ya Madini ya Margania na kufanikiwa kupunguza gharama kubwa.
Akitoa Shukrani zake Makamu wa Pili wa
Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Zanzibar ni miongoni mwa
Nchi kadhaa Duniani zinazoendelea kujikwamua Kiuchumi kwa kujenga
Miundombinu kadhaa ikiwemo ile bara bara ambayo hurahisisha mfumo wa
Mawasiliano.
Balozi Seif aliuomba Uongozi wa Kampuni
hiyo ya utengenezaji wa Madini ya Margania ya Nchini Uturuki kuandaa
Mpango Maalum utakaowawezesha Wahandisi wa Sekta ya Mawasiliano
Zanzibar kuiona Teknolojia hiyo na kuangalia mazingira ya Zanzibar
iwapo inaweza kutumika.
Alisema licha ya juhudi kubwa zinazoendelea
kuchukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya uimarishaji wa
Miundombinu ya Bara bara lakini bado zipo baadhi ya Bara bara Mjini na
Vijijini zinahitaji kuimarishwa kwa kutumia Teknolojia itakayoziwezesha
zidumu kwa kipindi kirefu.
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Post a Comment
karibu kwa maoni