0
Madereva pikipiki 'bodaboda' wametakiwa kuwa mstari wa mbele katika kufichua vijana wanaojishughulisha na shughuli za uhalifu kwa kutumia kivuli cha bodaboda ili kuondokana na na vitendo vya uhalifu.
Akizungumza na madereva wa pikipiki wa kijiji cha Kwa Mtoro wilayani Kondoa mkoani Dodoma wakati akifunga mafunzo ya usalama barabarani, Mkaguzi Msaidizi wa polisi Jackson Sizya amesema bodaboda wengi wamekuwa wakitumika vibaya katika kuchochea vitendo vya kiuhalifu hivyo ni muda sahihi kwa wao kujiweka mbali na matukio hayo.
"Mmekuwa mnatumiwa na wahalifu kwa sababu ni wepesi wa kukwepa ni vyema mkawa mabalozi wazuri wa vyombo vya dola kuwafichua wahalifu na siyo kushirikiana nao na kuwapeleka mafichoni. Hatutegemei nyinyi mlioshiriki mafunzo haya mkawabeba wahalifu kwenda hata kuvamia benki. Kwa sheria za Tanzania mtawachukuliwa wote adhabu sawa" alisema
Katika hatua nyingine mkaguzi huyo amewataka madereva wa pikipiki maarufu bodaboda kutumia vyema elimu ya usalama barabarani katika kuondokana na ajali za barabarani 
"Ni matumaini yangu kwamba mtaenda kupunguza ajali, kuokoa maisha ya watu wengine, na kusimamia usalama barabarani. Nendeni mkarejeshe amani kwa abiria wenu kwa kuanza safari salama na kumaliza salama siyo kutengeneza huzuni," aliongeza.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top