0
mediaRais wa Rwanda Paul Kagame, amekuwa katika ziara ya siku moja nchini Tanzania siku ya Jumapili, ikiwa ni ziara yake ya pili ya kikazi nchini humo tangu kuingia madarakani kwa rais John Magufuli mwaka 2015.
Katika mashauriano yake na mwenyeji wake rais Magufuli, viongozi hao wawili wamekubaliana kujenga reli ya kati kutoka Isaka nchini Tanzania hadi jijini Kigali.
Marais hao wamewaagiza Mawaziri wa nchi hizo mbili wanaohusika na uchukuzi kukutana hivi karibuni, kujadili uwezeshaji wa mradi huu mkubwa.
Rais Magufuli amesema mradi huu utaimarisha Jumuiya ya Afrika Mashariki kibiashara na kusaidia kuunda nafasi za kazi hasa kwa vijana.
Mradi huu ukikamilika, utasaidia wafanyibiashara kusafirisha mizigo kati ya nchi hizo mbili, hasa Rwanda ambayo itakuwa na uwezo wa kusafirisha kwa urahisi mizigo yake kutoka bandari ya Dar es salaam.
Uganda na Kenya pia zimekubaliana kujenga reli hiyo kutoka Malaba upande wa Kenya hadi jiji kuu Kampala.
Mbali na mradi huu, Tanzania na Uganda zinashirikiana katika mradi wa bomba la mafuta kutoka Hoima kwenda Bandari ya Tanga, mradi ambao ukikamilika, utasaidia Uganda kusafirisha mafuta yake katika soko la Kimataifa.
Mataifa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda, Burundi na Sudan Kusini yamekubaliana kuimarisha miundo mbinu ya reli na barabara ili kuunganisha eneo la Afrika Mashariki kwa lengo la kuimarika kiuchumi.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top