0
Waziri wa Maliasili na Utalii, Dk Hamisi Kigwangalla amesema vigogo watano ni miongoni mwa wanaotajwa kuwa ni kati ya watu 83 waliochukua maeneo na kujenga nyumba katika kiwanja cha Mamlaka ya Hifadhi Ngorongoro (NCAA), wakiwamo mawaziri wakuu wa zamani, Edward Lowassa na Frederick Sumaye.

Akizungumza na wajumbe wa bodi mpya ya NCAA aliyoizindua jana, Dk Kigwangalla alisema mwingine ni Daniel Ole Njoolay ambaye aliwahi kuwa mkuu wa Mkoa wa Arusha.

“Nimewataja hawa baadhi, najua kuna wengine, sasa naipa jukumu bodi na menejimenti kuendelea kuwataja na hatua za kurejesha ardhi zianze,” alisema.

Waziri huyo alisema tayari ameshamueleza Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi juu ya mgogoro huo.

Alisema anajua njama zilizotumika kugawa eneo hilo la ekari 20 kati ya 40 kwa kuwa jiji la Arusha lilikuwa halina uwezo wa kugawa eneo ambalo si lake.

“Jiji wamegawa eneo hili mwaka 1996 wakati likiwa chini ya umiliki wa Shirika la Taifa la Utalii lililobinafsishwa na NCAA walinunua hili eneo mwaka 2006,” alisema.

Lakini, mmoja wa wakazi wa eneo hilo, Juliana Peter alisema walipata viwanja hivyo baada ya jiji kutangaza kuvigawa wakifuata taratibu zote, “Mzazi wangu ndiye alinunua kiwanja na najua ana hati hivyo sisi si wavamizi.”

Mbali na kuitaka kufuatilia suala hilo la ardhi, Dk Kigwangalla ameitaka, “kusaidia kusimamia mali za NCAA lakini pia kuongeza siku za watalii kukaa Ngorongoro kutokana na kuongeza vivutio.”

“Pia mnapaswa kukaa na jamii kuboresha mahusiano ili ule mpango wa Ngorongoro wa miaka 10 ufanikiwe, hivyo mnapaswa kukaa na jamii kutafuta namna bora ya kujenga mahusiano kupitia miradi ya maendeleo,” alisema.

Dk Kigwangalla alirejea agizo lake kwa Jeshi la Polisi kutaka liwakamate watuhumiwa wanne kwa madai ya kushiriki katika mtandao wa ujangili ndani ya siku saba.

Alitoa agizo hilo Januari 25 na kusisitiza kwamba jeshi hilo likishindwa kuwakamata, atalishtaki kwa Amiri Jeshi Mkuu ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Dk Kigwangalla alisema jana kwamba anasubiri siku saba zifike na kama hatua zitakuwa hazijachukuliwa atafikisha suala hilo kwa Rais John Magufuli.

“Uamuzi wangu niliotangaza Januari 25 upo palepale nilitoa siku saba hazijafika ila zikifika kama hakuna hatua nitampelekea Rais jambo hili,” alisema.

Alisema ana imani kubwa na Polisi kuwa itazifanyia kazi taarifa alizotoa.

Hata hivyo, siku moja baada ya kutoa agizo hilo, msemaji wa jeshi hilo, Barnabas Mwakalukwa alisema halifanyi kazi kwa matamko, bali kwa kufuata kanuni, taratibu na sheria za kuanzishwa kwake.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top