0
Dkt Magufuli akiweka saruji iliyochanganywa na kokoto kwenye jiwe hilo la msingi la ujenzi wa Reli ya Kisasa eneo la Ihumwa stesheni mkoani Dodoma.Rais wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli amewahimiza raia nchini humo wazaane bila kuwa na wasiwasi.
Amesema anaamini watu wakiwa wengi ndivyo wanavyokuwa na usemi zaidi, hasa katika jumuiya za kiuchumi.
Dkt Magufuli alisema hayo alipokuwa anaweza ameweka jiwe la msingi la kipande cha pili cha mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa maarufu kama Standard Gauge Jumatano.
Sehemu hiyo ya reli inaanzia Morogoro hadi Makutupora Mkoani Dodoma.
"Tanzania tuna bahati sana kutokana na ukubwa wa nchi yetu, hivi karibuni tumeambiwa tumefika 55 milioni. Wapo waliosema kwanini milioni 55 tunazaana mno, mimi nasema tuzaane zaidi kwa maana mnapokuwa wengi mnakuwa na sauti hata kwenye jumuiya mlizonazo," alisema Dkt Magufuli alisema kwa mujibu wa runinga ya EATV na gazeti la Nipashe.
"Nchi ya China ina watu bilioni 1.3 na ndio maana sasa hivi uchumi wake upo juu, mkiwa wengi mnakuwa na sauti, idadi ya watu wetu ni sauti tosha katika Jumuiya ya Afrika Mashariki. Tunachotakiwa ni sisi Watanzania tuchape kazi."
Dkt Magufuli alisema jambo muhimu si wingi wa watu bali ni kwa njia gani wananchi wanashiriki katika shughuli za maendeleo.Magufuli
"Nchi ya Denmark ina watu milioni tano lakini kwa sababu ya uchapakazi wao wamekuwa wakitoa msaada mpaka kwenye nchi kama Tanzania yenye watu 55 milioni.
"Kwa hiyo jukumu letu tulionalo ndugu zangu tusiogope kuwa wengi, tukubali kuwa wengi, lakini wanaochapa kazi".
Wakati wa sherehe hiyo ya kuweka jiwe la msingi, Dkt Magufuli pia aliwaahidi kwamba ujenzi wa reli hiyo ya kisasa itabadilisha sana uchukuzi Tanzania.
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Reli Tanzania (TRC) Bw Masanja Kadogosa, akizungumza wakati wa uzinduzi huo, alisema ujenzi wa kipande cha pili cha reli chenye urefu wa kilometa 422 utagharimu Shilingi Trilioni 4.3.
Ujenzi wa kipande hicho cha pili utakaofanyika kwa miezi 36 utakamilika ifikapo tarehe 25 Februari, 2021.
Ni sehemu ya mradi mkubwa ujenzi wa reli ya kati wa kuanzia Dar es Salaam hadi Mwanza yenye urefu wa kilometa 1,219.
Ujenzi wa kipande cha kwanza cha kuanzia Dar es Salaam hadi Morogoro ulianza mwishoni mwa mwaka 2016 na unatarajiwa kukamilika Novemba 2019.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Makame Mbarawa Mnyaa alisema ujenzi wa kipande cha kwanza umefikia asilimia 9.
Kwa mujibu wa Prof Mbarawa, treni zitakazotumia reli hiyo zitakuwa na uwezo wa kubeba tani 10,000 za mzigo kwa wakati mmoja.
Mizigo ya tani 10,000 ingesafirishwa malori 500 ambayo yangesafirisha mzigo kwa barabara.
Kwenye reli hiyo, treni itakuwa na uwezo wa kwenda kasi ya kilometa 120 kwa saa na treni ya abiria kwenda kwa kasi ya kilometa 160 kwa saa.
Rais Magufuli alielezea kufurahishwa na utekelezaji wa mradi huo na kusema kando na kurahisisha na kupunguza gharama za usafirishaji wa mizigo na abiria, na pia utaokoa barabara ambazo zinaharibika kutokana na kusafirishaji mizigo mizito kwa magari.
Rais huyo alisema reli hiyo itakuwa na uwezo wa kusafirisha tani milioni 17 za mizigo kwa mwaka ikilinganishwa na ya sasa yenye uwezo wa kusafirisha tani milioni 5 tu.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top