0
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Vijijini,Mkoani Manyara , Hudson Stanley Kamoga, amewataka  watendaji,madiwani na wananchi kumpa ushirikiano katika utendaji  wa kazi ya kuwatumikia wananchi Wilayani  humo kwa lengo la kusukuma gurudumu la maendeleo.
 Akiongea na waandishi wa habari Jana ofisini kwake,Kamoga alisema  ushirikiano katika nyanja yoyote ile inahitajika ili kufikia malengo,hivyo naye anaomba apewe ushirikiano ili kuweza kufikia malengo aliyojiwekea katika kuhakikisha wilaya hiyo inapata maendeleo ya kweli na si vinginevyo.

 Kamoga alisema ushirikiano huo uende sambamba na kuwataka wakuu wa idara  kumpa mpango  wa mwezi mmoja ikiwa ni utekelezaji katika kuhakikisha kila mkuu wa idara anasimamia majukumu yake ipasavyo.
 Alisema yeye kama Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Mbulu, angependa kuona madiwani na watendaji wa halmashauriya wilaya hiyo  wakiwa wanazungumza lugha moja tu ya maendeleo na si vinginevyo.
"Lazima kama Mkurugenzi mtendaji wa  halmashauri ya wilaya ya Mbulu,nihakikishe  watendaji na madiwani wanafanya kazi kama timu moja, kwani siku zote umoja ndio hujenga kitu chochote cha maendeleo na msingi wa maendeleo ni ushirikiano yaani umoja,hivyo uwezo ninao wa kulisimamia hili na hatimaye kuweza kuona tuko wapi, tumetoka wapi na tunatarajia kwenda wapi " alisema Kamoga.
 Pia alisema ili kufikia malengo aliyojiwekea kikamilifu,  ametengeneza utaratibu ambapo angependa watendaji wake wote wa halmashauri waufuate na kuuzingatia kikamilifu katika utekelezaji wa majukumu yao ya Kila siku.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top