0
Benny Mwaipaja, WFM, Dar es Salaam
Displaying IMG_8462.JPGWaziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango ameitaka nchi ya Uingereza kutazama uwezekano wa kufanya biashara na Tanzania kwa kununua bidhaa zilizoongezwa thamani badala ya hali ya sasa ambapo nchi hiyo imekuwa ikinunua bidhaa ghafi ilihali ikiingiza nchini bidhaa zake za viwandani.
Dkt. Mpango ameyasema hayo alipokutana na Mjumbe wa Waziri Mkuu wa Uingereza anayeshughulikia masuala ya Biashara Bw. Lord Hollick ailipo tembelea Makao Makuu ya Wizara hiyo jijini Dar es salaam.
Amesema Tanzania inataka kuona inauza bidhaa zake zenye thamani ambazo zitatokana na maendeleo makubwa ya viwanda hapa nchini ikiwa ni Sera ya nchi kuwa na uchumi wa kati unaotegemea viwanda ifikapo mwaka 2025.
Nchi ya Uingereza imekuwa ikifanya biashara na Tanzania kwa kiasi kikubwa na takwimu zinaonesha nchi hiyo inaingiza bidhaa zenye thamani mara nane ya Tanzania jambo ambalo linatakiwa kurekebishwa ili biashara iwe na manufaa kwa pande zote mbili.
Miongoni mwa bidhaa ghafi ambazo zimekuwa zikisafirishwa kwenda uingereza ni pamoja na Chai, kahawa na madini ya vito huku Uingereza ikiingiza bidhaa za viwandani zenye thamani kubwa ikijumuisha mashine (mitambo),vifaa vya umeme, bidhaa za plastiki na madawa.
Kwa upande wake, Mjumbe wa Waziri Mkuu wa Uingereza anayeshughulikia Biashara Bw. Lord  Hollick amebainisha nia ya nchi yake kutaka kuwekeza kwa kiasi kikubwa katika nchi za Afrika ikiwemo Tanzania baada ya Taifa hilo kuamua  kujiondoa katika Umoja wa Ulaya.
Maeneo ambayo Uingereza inapenda kuwekeza Tanzania ni katika Sekta ya Kilimo, Nishati ya Umeme na Usafirishaji huku kwa sasa akionesha nia ya ya nchi yake kuwekeza katika ujenzi wa kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Msalato katika Makao Makuu ya nchi - Dodoma. 
Pia nchi hizo mbili zimekubaliana kuandaa mkutano utakao wakutanisha Serikali na Sekta Binafsi ya Tanzania kwa upande mmoja na wawekezaji wakubwa kutoka Uingereza na nchi nyingine za Ulaya ambao utasaidia kukuza uwekezaji na biashara na kufungua fursa mbalimbali za kiuchumi kwa manufaa ya wananchi wa Tanzania na  nchi hizo za Ulaya ikiwemo Uingereza. 

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top