0


Displaying IMG_2322.JPGSERIKALI imepokea gawio la zaidi ya shilingi bilioni 10 kutoka taasisi tatu ikiwemo TPB bank, na kampuni mbili za mafuta za Tiper na Puma ambazo serikali inamiliki hisa zake.

Taasisi ya kwanza kuwasilisha gawio hilo kwa Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango mjini Dodoma ni Benki ya TPB ambayo mwenyekiti wake Profesa Lettice Rutashobya amekabidhi hundi kifani ya shilingi bilioni 1.032, ikifuatiwa na Kampuni ya kuhihadhi mafuta ya Tiper iliyowasilisha gawio la shilingi bilioni 2.

Kampuni ya mafuta ya Puma ikahitimisha zoezi hilo kwa kukabidhi hundi kifani ya shilingi bilioni 7 ambazo ni sehemu ya faida ya shilingi bilioni 14 ambazo kampuni hiyo imepata baada ya kulipa kodi.

Akizungumza katika tukio hilo lililofanyika Makao Makuu ya Wizara ya Fedha na Mipango Mjini Dodoma, Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango amezipongeza taasisi hizo na amezitaka Taasisi za Serikali na mashirika ya umma kuilipa Serikali gawio la hisa zake na zijiendeshe kwa ufanisi na kwa faida ili makusanyo hayo yaweze kuwahudumia wananchi.

Dkt. Mpango amerejea kauli yake aliyoitoa bungeni mjini Dodoma wakati akiwasilisha Bajeti Kuu kwamba Serikali itatoa kipaumbele kwa kufanya biashara na taasisi zake za Umma ili ziweze kujiimarisha kimapato na hatimaye kutoa gawio Serikalini.

“Leo ni siku nzuri sana kwa watanzania kwa sababu Serikali inapokea gawio la shilingi bilioni 10 kwa niaba yao lakini fedha hizi hazitoshi nataka mfanye vizuri zaidi ili gawio liweze kuongezeka ili tuzielekeze kutatua kero zinazoikabili jamii ikiwemo elimu, afya na maji” alilisisitiza Dkt. Mpango.


Katika tukio hilo pia, Benki ya TPB Plc imelipatia Shirika la Posta kiasi cha shilingi milioni 97.8 ikiwa ni gawio kulingana na hisa zake asilimia 7.98 inazomiliki katika Benki hiyo.

Akipokea hundi kifani ya kiasi hicho cha gawio, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Posta nchini, Dkt. Haruni Ramadhan Kondo, ameiomba Serikali ililipe shirika lake kiasi cha shilingi bilioni 3.6 ambazo ni malipo ya pensheni ya wastaafu wa lililokuwa Shirika la Posta na Simu la Jumuiya ya Afrika Mashariki ambapo Shirika limelipa pensheni hizo kwa niaba ya Serikali ili liweze kuongeza mtaji na kujiendesha kwa faida zaidi.

Awali Wenyeviti wa Bodi za wakurugenzi wa Taasisi hizo wameahidi kuendelea kufanya biashara kwa umahili mkubwa ili kuongeza gawio kwa wanahisa wake na kuiomba iwawekee mazingira yatakayosaidia kufanikisha azma yao hiyo.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TPB Bank, Profesa Lettice Rutashobya, amesema kuwa Benki yake imeendelea kukua kwa kasi, kuimarika na kufanya vizuri katika biashara ya fedha pamoja na kuwa mahili katika ubunifu na kuwa tishio kwa taasisi nyingine za fedha.

Nae Meneja wa Kampuni ya Kuhifadhi Mafuta-Tiper, Bw. Emmanuel Kondi, ameiomba Serikali kuiwezesha kampuni hiyo kufanya biashara kwa mafanikio zaidi hivyo kuongeza gawio ikiwemo kuangalia upya mfumo wa himaya moja ya Forodha ambao amesema pamoja na kuwa na ufanisi mkubwa una baadhi ya changamoto.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Kampuni ya Kuuza Mafuta-Puma, Dkt. Ben Moshi amesema kuwa Kampuni yake ilitengeneza faida na kuiwezesha kutoa gawio la shilingi bilioni 7 kwa Serikali ikilinganishwa na shilingi bilioni 4.5 ilizotoa mwaka wa fedha uliopita.


Utaratibu wa Taasisi za Serikali na mashirika ya umma kulipa gawio la hisa kwa Serikali na wanahisa wengine ni maelekezo ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ya kuhakikisha kuwa Taasisi hizo zinafanya kazi kwa ufanisi, kuzalisha faida na kutoa gawio kwa Serikali ili mapato hayo yaweze kuhudumia wananchi katika Nyanja mbali mbali kama vile huduma za afya, elimu, maji na barabara.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top