0
Mkuu wa Mkoa wa Manyara Alexander Mnyeti amewataka watu wote wanaomiliki silaha mkoani Manyara kuzisalimisha katika vituo vya polisi na kufanya utaratibu kuzisajili upya kutokana na baadhi ya watu kutumia silaha hizo kufanya mauaji katika migogoro inayojitokeza ya mipaka kati ya wilaya ya Kiteto na Kilindi.

Mnyeti amesema kuwa tayari ametoa maagizo kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara kufanya uhakiki wa silaha hizo ili kudumisha hali ya ulinzi na usalama katika mkoa huo hususan maeneo yenye migogoro .

Mkuu wa Mkoa wa Tanga Martini Shigela akizungumza katika utatuzi wa Mgogogoro  wa mpaka kati  ya Wilaya ya Kilindi iliyoko mkoani Tanga na Wilaya ya Kiteto iliyoko mkoa wa Manyara amesema kuwa kuna watu wanaomiliki silaha kiholela bila kufuata sharia na wamekua waitumia silaha hizo kufanya uhalifu na kugharimu maisha ya watu hivyo serikali haitawavumilia kwani hatua kali zitachukuliwa kwa watakao bainika.

Waziri wa Ardhi,Nyumba na Makazi ,Wiliam Lukuvi amesema kuwa Wizara yake imeamua kutatua mgogoro huo kama Waziri Mkuu alivyoagiza hivyo wataweka alama za kitaalamu za nukta zinazotambulika kimataifa zisizotumia vitu vinavyohamishika ili kuepusha migogoro kati wilaya hizo ikiwa ni pamoja na kuanisha mpango wa matumizi bora ya ardhi utakaosaidia kuepusha migongano isiyo na tija.

Waziri wa Ofisi ya Raisi Tawala za Serikali za Mitaa Suleman Jafo amesema kuwa kwa pamoja wamekubaliana na viongozi kumaliza mgogo huo ambao umegharimu maisha ya watu wengi na kudumu kwa miaka mingi ili kuhakikisha kuwa wananchi wanajikita katika shughuli za kujiletea maendeleo badala ya kuendekeza migogoro.

Kwa upande wao Wananchi wa Wilaya ya Kiteto na Kilindi  Mwajuma Bakari .na Mohamed Chambali wamesema kuwa kutatuliwa kwa mgogoro huo kutasaidia kuepusha vitende vya mauaji ya watu wasiokua na hatia ambavyo husababishwa na migogoro hiyo ,hivyo wameiomba serikali iendeleze juhudi za utatuzi wa migogoro katika maeneo mengi nchini

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top