0
Image result for mji wa BABATI 
Hali ya mapato ya Halmashauri ya Mji wa Babati mkoani Manyara imeelezwa kuwa sio nzuri kulinganisha na matumizi ambapo matumizi ya kawaida ya kulipa umeme, maji, usafi na matumizi mengine yanakaribia shilingi milioni 200 kwa mwezi huku mapato ni wastani wa shilingi milioni 140.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Babati, Mohamedy Kibiki alibainisha hayo katika kikao cha Baraza la Madiwani kilichokuwa kikitathimini  hali ya ukusanyaji wa mapato katika vyanzo vya mapato vya halmashauri hiyo ili viende sambamba na utoaji huduma kwa wananchi.

Alisema kasi ya ukusanyaji wa mapato ni lazima iboreshwe ili ilingane na matumizi kwani huwezi kukusanya kidogo na kuwa na matumizi makubwa halmashauri hiyo itakwama na itashindwa kujiendesha na kuendesha vikao mbalimbali.

“Hali sio nzuri tunatakiwa tutoke hapo,tuhakikishe tunasimamia na kuboresha mapato ya Halmashauri yetu,mapato hayo yataendelea kushuka ikiwa  hatutakuwa wabunifu na kuacha kufanyakazi kwa mazoea” Alisema Kibiki.
 “Ni muhimu tuwe wabunifu, tuboreshe vyanzo vya mapato na kubuni vyanzo vipya ili kupunguza mzigo wa ukusanyaji fedha na hatimaye kuweza kutoa huduma stahiki kwa wananchi”. Alisema.
 
Wananchi wanaweza kuhoji Halmashauri yoyote kwa kushindwa kuwatolea huduma stahiki pamoja na kufanya vikao vya kikatiba vinavyohusu maendeleo ya eneo lao.

Alibainisha kuwa madiwani wakishirikiana na watalaamu wataweza kusimamia kikamilifu suala la uvamizi wa maeneo ya shule kwa kupima eneo hilo, uvamizi wa viwanja vilivyopimwa katika eneo la Makatanini na kuepusha migogoro inayoweza kuepukika.

Pia kufuatilia ujenzi holela wa vichochoro mbalimbali vilivyovamiwa na wananchi na  kujenga stoo za kuhifadhia vifaa, uzoaji wa taka ngumu katika vizimba na kuondoa karakana bubu katikati ya mji huo ili kuboresha afya za wakazi wa mji huo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji wa Babati,Fortunatus Fwema aliliambia Baraza hilo kuwa Halmashauri hiyo haina vyanzo vingi vya mapato jambo ambalo husababisha kushindwa kuendeleza miradi ya maendeleo na kubaki kusubiri  ruzuku kutoka Serikali kuu ambazo huja kwa maelekezo maalum.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top