SERIKALI imesema imeanza mchakato wa kuajiri watumishi 52,436 wanaohitajika katika kada mbalimbali nchini.
Hayo
yalielezwa bungeni mjini Dodoma na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -
Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Mkuchika
alipowasilisha hotuba yake kuhusu makadirio ya bajeti ya wizara hiyo kwa
mwaka ujao wa fedha.
Alisema
uhakiki wa mahitaji ya rasilimali watu katika utumishi umma ikiwamo
mikoa yote, umefanyika kupitia Mfumo wa HCMIS na kubaini idadi hiyo ya
mahitaji ya watumishi wa kada mbalimbali.
"Serikali
imeanza mchakato wa kuajiri watumishi hao kwa kuzingatia maeneo ya
kipaumbele na kuimarisha kada zenye upungufu mkubwa," alisema.
Mkuchika
ambaye pia ni Mbunge wa Newala, alibainisha kuwa kada ya afya ina
upungufu wa watumishi 14,102, elimu 16,516, kilimo 1,487, mifugo 1,171
na uvuvi 320.
Aliongeza
kuwa polisi kuna upungufu wa watumishi 2,566, magereza 750, uhamiaji
1,500, zimamoto 1,177, hospitali za mashirika ya kidini na hiari 174 na
wengineo 12,673.
Mkuchika
alisema kuwa katika mwaka huu wa fedha, usimamizi wa ajira za watumishi
wa umma umefanyika kwa waajiri wote ambapo watumishi wapya 15,000
wameajiriwa, wakiwamo jumla ya walimu 4,348 wa masomo ya sayansi na
watumishi 3,152 wa kada ya afya ili kuziba pengo lililosababishwa na
kuondolewa kwenye Orodha ya Malipo ya Mishahara kwa watumishi wa umma
waliobainika kughushi vyeti.
"Maofisa
utumishi 1,595 wamechukuliwa hatua za kinidhamu ikiwamo kufungiwa
dhamana ya kuingia katika mfumo wa HCMIS, kufikishwa mahakamani na
wengine kesi zao zipo Takukuru," alisema Mkuchika.
Post a Comment
karibu kwa maoni