0
Na Teresia Mhagama, Manyara
Waziri wa Nishati Medadi Kalemani akiwasha umeme katika kijiji cha Tango mjini Mbulu.
Wananchi katika kijiji cha Tangomtimkubwa  katika Wilaya ya Mbulu  na Kijiji cha Dudiye  wilayani   Babati mkoa  wa Manyara,  wameanza kupata huduma ya umeme baada ya Waziri wa Nishati, Dkt Medard Kalemani kuizindua tarehe 8 Mei, 2018.
Dkt. Kalemani aliwasha umeme katika vijiji hivyo akiwa katika ziara mkoani Manyara  katika wilaya hizo ambapo alikagua utekelezaji wa mradi wa usambazaji umeme vijijini Awamu ya Tatu (REA III) pamoja na miradi mingine ya umeme mkoani humo.
Katika ziara hiyo,  Dkt Kalemani alieleza kuwa, kutokana   na wananchi wengi vijijini kuhitaji huduma ya umeme, Serikali imeamua kuongeza zaidi ya vijiji 72 vya mkoa huo katika mpango wa kusambaziwa  umeme kupitia REA III mzunguko wa kwanza utakaokamilika Juni 2019.
"Awali mkoa wa Manyara ulipewa vijiji 142 ambavyo vinapaswa kusambaziwa umeme katika mradi wa REA III mzunguko wa kwanza lakini baada ya kufanya tathmini tumeongeza vijiji zaidi ya 72 ambavyo usambazaji wake wa umeme unapaswa kukamilika ndani ya muda uleule uliopangwa ambao ni Juni 2019," alisema Dkt Kalemani.
Dkt. Kalemani alisema kuwa, maeneo mengi zaidi yanahitaji kusambaziwa umeme katika mkoa wa Manyara  kwani matumizi ya umeme mkoani humo ni  madogo kulinganisha na kiasi cha umeme kinachopatikana ambapo alisema kuwa, matumizi ya umeme ni chini ya asilimia 30.
Kuhusu uboreshaji wa miundombinu ya umeme mkoani humo unaojumuisha uondoaji wa miundombinu chakavu, Dkt Kalemani aliwaagiza watendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) katika mkoa huo kuhakikisha kuwa wanakamilisha kazi hiyo ifikapo mwezi Juni mwaka huu ili wananchi wapate umeme wa uhakika.
Akiwa wilayani Mbulu, Dkt. Kalemani pia alizungumza na wananchi wa kijiji cha Maretadu katika Jimbo la Mbulu Vijijini ambapo aliwaahidi kuwa huduma ya umeme kijijini hapo itapatikana kuanzia tarehe 12 Juni, 2018.
Awali akitoa taarifa ya usambazaji umeme vijijini katika mkoa huo, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Manyara ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Babati, Raymond Mushi alisema kuwa,  mradi wa usambazaji umeme vijijini Awamu ya Pili katika mkoa huo umekamilika ambapo asilimia 96.3 ya wananchi waliunganishwa na huduma ya umeme.
Kuhusu Mradi wa usambazaji umeme vijijini Awamu ya Tatu (mzunguko wa kwanza), alisema kazi zinazoendelea ni kuchimba mashimo,  kusimamisha nguzo na kuvuta nyaya katika vijiji vitano ambapo vijiji vitatu tayari vimeshawashiwa umeme.
Katika ziara hiyo,  Dkt. Kalemani aliambatana na Mbunge wa Mbulu Mjini, Issaay Zacharia, Mbunge wa Mbulu Vijijini, Flatei Massay na Mbunge wa Babati Vijijini, Jitu Soni.
Pamoja na kupongeza juhudi za Serikali katika usambazaji umeme vijijini, Wabunge hao walieleza kuwa vijiji vingi katika Majimbo hayo bado havijasambaziwa umeme hivyo Serikali iweke mkazo katika kuhakikisha kuwa Mkandarasi anakamilisha kazi kwa wakati ili kuwawezesha wananchi kujiendeleza hasa kiuchumi.
Kwa upande wake, Mbunge wa Babati Mjini, Pauline Gekule, pamoja na  kupongeza mradi wa usambazaji umeme vijijini na watendaji wa TANESCO mkoani Manyara, aliomba Serikali kuongeza vifaa vya usambazaji umeme  kama vile nguzo ili watendaji wa TANESCO wasambaze umeme kwa kasi.
 
Waziri wa Nishati Medadi Kalemani baada ya kukata utepe kuashiria kuwashwa kwa Umeme katika kijiji cha Tango wilaya ya Mbulu mkoani Manyara ikiwa ni Rea awamu ya Tatu huku akimtaka mkandarasi pamoja na Tanesco kuhakikisha kila nyumba inafungiwa Umeme.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top