0
Waziri wa Mambo ya Nje Nchi, Dkt Augustine Mahiga amekiri Tanzania imepunguza uhusiano wa kibiashara na nchi  ya Korea Kaskazini tangu mwaka 2014 hivyo Tanzania imeshtushwa baada ya kutajwa miongoni mwa nchi ambazo zimechunguzwa na Umoja wa Mataifa.
Akizungumza leo na wanahabari jijini Dar es salaam , Mh. Waziri amesema licha ya uhusiano uliokuwepo awali, lakini tangu mwaka huo Tanzania imepunguza kabisa uhusiano wa kibiashara na kidiplomasia ingawa hakuna ugomvi, na kusema kitendo cha kuhusishwa kuwa na uhusiano wa kibiashara na nchi hiyo kimeishtua serikali
"Hatuna ugomvi na Korea Kaskazini, lakini kitendo chao cha kutengeneza silaha za kuangamiza siyo kizuri  kwa heshima na usalama wa dunia. Ndiyo maana tukaanza kuchukua hizo hatua za kupunguza mahusiano tangu 2014,"  amesema 
Mh. Mahiga amefafanua kuwa awali uhusiano wa kibiashara ulikuwepo kabla ya vikwazo vilivyowekwa hivi karibuni na Baraza la Umoja wa Mataifa.
Inadaiwa kuwa Tanzania na Uganda ni miongoni mwa baadhi ya nchi zinazochunguzwa na Umoja wa Mataifa kwa tuhuma za kwenda kinyume na vikwazo vilivyowekwa na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa dhidi ya Korea Kaskazini. 
Hata hivyo ripoti ya uchunguzi huo ilitolewa Septemba 9, 2017 ambapo Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilisema linachunguza tuhuma za Tanzania kuingia mikataba ya kijeshi na Korea Kaskazini inayogharimu dola za kimarekani milioni 12.5.
Pamoja na hayo Waziri  Mahiga amesema kuwa  anaelekea katika mkutano wa kawaida wa Umoja wa Mataifa na akiwa huko atatumia fursa hiyo kujibu tuhuma hizo kwa Baraza la Usalama.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top