0
Baada ya kutokuwa na mwenendo mzuri na kikosi cha Mbao FC msimu huu, inaelezwa kuwa Kocha Ettiene Ndayiragije, ameikacha timu na kutimkia kwao Burundi.

Kocha huyo hakuonekana katika benchi la ufundi jana dhidi ya Majimaji FC huku Msaidizi, Flugence Novatus akisimamia kuiongoza timu katika mchezo uliomalizika kwa sare ya mabao 2-2.

Mara ya mwisho Ndayiragije kuiongoza Mbao FC ilikuwa ni dhidi ya Lipuli FC iliyomalizika kwa matokeo ya 0-0 huku mashabiki wakimuandama aiachie timu ambapo baada ya mtanange huo kumalizika alipewa ulinzi na askari.

Taarifa zilizo chini ya kapeti kutoka Mbao zinaeleza kuwa tayari Kocha huyo ameshaondoka huku Novatus akikaimu nafasi kwa muda.

Mbao ipo nafasi ya 12 kwenye msimamo wa ligi msimu huu kwa kujikusanyia pointi 24 ikiwa imecheza mechi 25.

Hivi karibuni, mashabiki walivamia uwanja baada ya mechi wakidai kocha huyo alipanga wachezaji kadhaa akiacha walio muhimu nje.

Post a Comment

karibu kwa maoni

 
Top